Azam FC imeanza vizuri michuano ya Kombe la Shirikisho ya Caf kwa kuitwanga Bidvest Wits ya Afrika Kusini mwa mabao 3-0 ikiwa nyumbani kwao Afrika Kusini.

Azam FC ambayo ilitua nchini humo siku tatu zilizopita, ilikwenda mapumziko na  sare ya bila kufungana dhidi ya wenyeji wake.

Azam FC ambao walianza kipindi cha kwanza kwa tahadhari kubwa walionekana kubadilika katika kipindi cha pili na kushambulia mfululizo hadi walipopata bao katika dakika ya 51 kupitia Salum Abubakary ‘Sure Boy’ aliyepiga shuti kali nje ya 18.


Wakati Wits wanajiuliza, Azam FC haraka ilipata bao la pili kupitia Shomari Kapombe ambaye alifanya juhudi kulala chini na kuuwahi mpira wa krosi aliousukumiza wavuni.

Bao la pili la Azam FC lilionekana kuwachanganya Wits, Azam FC wakaitumia nafasi hiyo kusukuma mashabulizi mfululizo na dakika ya 59, ikaandika bao lake la tatu kupitia kwa nahodha John Bocco, ‘Adebayor’.


Dakika ya 73, kocha Stewart Hall alimtoa Didier Kavumbagu na nafasi yake ikachukuliwa na Khamis Mcha, dakika ya 79 akamtoa Kapombe na kumuingiza Waziri Salum na dakika ya 83 akamtoa Kipre Bolou na nafasi yake akaichukua Frank Domayo.

Advertisement

 
Top