simba
Gemu ya kwanza ya Simba msimu huu itakuwa ni ile dhidi ya African Sport katika uwanja wa Mkwakwani, Tanga siku ya Jumamosi hii. Watacheza na JKT Mgambo siku tatu baadae katika uwanja huo huo wa Mkwakwani.  
UWANJA MGUMU KWAO…
Kwa misimu miwili iliyopita Simba imeshindwa kupata ushindi katika mchezo wa kwanza wa msimu. Walilazimisha sare ya 2-2 katika uwanja wa Ally Hassan Mwinyi, Tabora dhidi ya Rhino Rangers ya Tabora ambayo ilikuwa ikicheza mchezo wake wa kwanza wa ligi kuu msimu wa 2013/14.
Coastal Union ya Tanga ilitoka nyuma kwa magoli 2-0 na kutengeneza sare ya 2-2 katika uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo wa kwanza wa Simba msimu uliopita. Sasa wanakwenda kuivaa timu ya African Sport ambayo itakuwa ikicheza mchezo wa kwanza wa ligi kuu baada ya kusubiri kwa miaka 23.
Simba haijawahi kushinda katika uwanja wa Mkwakwani katika gemu 6 zilizopita. Imetoa sare mara nne na kupoteza michezo miwili. Sports wanaweza kuishinda Simba?. Wana kila sababu ya kushinda, kupata matokeo ya sare lakini kupoteza itakuwa ni sawa na mwanzo mbaya katika uwanja wa nyumbani mbele ya timu ambayo haina rekodi ya kuvutia kwenye uwanja huo.
Sports haina wachezaji wenye majina makubwa lakini wamejipanga vizuri kiutawala huku wakiwaongeza wachezaji wazoefu kama Zahoro Pazzi, chini ya mwalimu Mlage Kabange timu hiyo ya Tanga itaendeleza rekodi ya Simba kutoshinda Mkwakwani Stadium.
MECHI 6 BILA BAO MKWAKWANI, MGAMBO NI ‘NUKSI KWAO’…
Mechi ya pili ya msimu Simba wataivaa JKT Mgambo ambayo katika misimu yake mitatu katika ligi kuu haijawahi kupoteza dhidi ya Simba ndani ya uwanja wa Mkwakwani. Licha ya kupoteza gemu zote walizowahi kucheza na Simba jijini Dar es Salaam tena kwa idadi ya 6-0, 4-0, Mgambo imeichapa Simba mara mbili katika gemu tatu za Tanga.
Walitoa suluhu-tasa msimu wa 2012/13, wakashinda 1-0 msimu wa 2013/14, wakashinda tena 2-0 msimu uliopita. Mara zote hizo Simba haijafanikiwa kufunga goli. Pia timu hiyo ya Dar es Salaam haijawahi kupata goli katika sare tatu mfululizo walizopata dhidi ya timu nyingine ya mkoa wa Tanga ndani ya misimu mitatu iliyopita.
MECHI YA KWANZA UWANJA WA TAIFA…
Kagera Sugar sasa ipo chini ya mwalimu mshindi wa tuzo ya kocha bora wa ligi kuu bara msimu uliopita, Mbwana Makatta. Timu hiyo ya Bukoba itacheza na Simba katika mchezo wa mzunguko wa tatu ndani ya uwanja wa Taifa. Simba itakuwa ikicheza gemu ya kwanza nyumbani msimu huu tena wakiwa wametoka katika uwanja mgumu wa Mkwakwani, Tanga.
Inaweza kuonekana mechi rahisi kwa kikosi cha Kerry lakini inaweza kuwa mechi ya kwanza ‘ngumu kuliko’ licha ya kwamba watakuwa katika uwanja wa nyumbani. Kushindwa kufunga goli/magoli katika gemu dhidi ya Sports na Mgambo ni jambo ambalo litaleta presha kwa timu hadi kwa mashabiki ‘wakereketwa’ wa klabu.
Kagera imefunga magoli manne katika gemu mbili za mwisho dhidi ya Simba katika uwanja wa Taifa na hawajapoteza mchezo wowote. Simba watakuwa na presha kwani gemu ya nne ni dhidi ya mahasimu wao Yanga SC. Kabla ya kuwavaa Yanga watakuwa wamekusanya pointi ngapi? Wanaweza kupata alama moja ama mbili katika michezo miwili ya Tanga na Kagera wanaweza kuondoka na alama tatu au moja katika mchezo wao wa mzunguko wa tatu.

Advertisement

 
Top